Sitta Awashukia Wadokozi Bandarini Wasipewe Dhamana, Awaita Wahujumu Uchumi - MULO ENTERTAINER

Latest

29 Jan 2015

Sitta Awashukia Wadokozi Bandarini Wasipewe Dhamana, Awaita Wahujumu Uchumi

Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta amesema angependa kuona sheria inayataja makosa ya udokozi bandarini kama ya uhujumu wa uchumi ili watuhumiwa wanapokamatwa na kushtakiwa wasipewa dhamana.

Waziri Sitta alisema hayo jana wakati akizungumza na watendaji wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), katika mfululizo wa ziara zake kwa mashirika, taasisi na mamlaka zilizo chini ya wizara yake kwa lengo la kufahamiana na kujua changamoto na kupanga mikakati yake katika utendaji.

Akizungumza katika mkutano na watendaji TPA, baada ya kusikiliza taarifa ya utendaji kazi iliyohusisha mikakati, mafanikio na changamoto za mamlaka hiyo, Sitta alisema duniani kote bandari ni kitovu cha uchumi wa nchi.

Alisema vitendo vyovyote vya udokozi na hujuma vinavyofanywa na watumishi wasio waaminifu ni kuhujumu uchumi wa Taifa, hivyo angependa kuona wahusika wanashtakiwa na kunyimwa dhamana.

Akizungumzia utendaji, Waziri Sitta aliwataka wote wenye mamlaka ya kufanya uamuzi kwa mambo mbalimbali wafanye hivyo bila woga wala kusubiri kushauriana na mamlaka nyingine.

“Nimekuja kuwaimarisha katika kufanya uamuzi, tuliowapa mamlaka lazima wawe na uamuzi wa haraka lakini uwe sahihi,” alisema Sitta.

Alisema katika kipindi cha miezi 10 kilichobaki cha uhai wa Serikali, ana kazi ya kufanya katika wizara hiyo ili wananchi waone mafanikio makubwa.

Awali, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TPA, Madeni Kipande alisema bandari imekuwa na mchango mkubwa katika uchumi wa nchi, kwani inachangia kati ya asilimia 35 hadi 40 ya mapato ya Serikali. Alisema mapato yaliongezeka kutoka Sh389 bilioni mwaka 2011/2013 hadi kufikia Sh539.7 bilioni mwaka 2013/2014.