Kwa Polisi Awatoroka Polisi na Kujirusha ghorofani - MULO ENTERTAINER

Latest

15 Sept 2015

Kwa Polisi Awatoroka Polisi na Kujirusha ghorofani

POLISI Kanda Maalumu ya Dar es Salaam imewakamata watuhumiwa 26 wanaojihusisha na vitendo vya ugaidi, huku Ally Ulatule anayetajwa kama kinara wa vikundi hivyo akijaribu kutoroka au kujiua kwa kujirusha kutoka ghorofa ya tatu wakati akihojiwa na polisi.

Aidha, Polisi Kanda hiyo kwa kushirikiana na vikosi maalumu tangu ianze operesheni ya kuwasaka watuhumiwa waliovamia vituo vya Polisi na kujihusisha na ugaidi, wamefanikiwa kuwakamata jumla ya watuhumiwa wanaojihusisha na vitendo hivyo 64 huku silaha 27 zilizoporwa katika vituo mbalimbali vya polisi zikipatikana.

Akizungumza na waandishi wa habari jana ofisini kwake, Kamanda wa Kanda hiyo, Kamishna Suleiman Kova alisema, katika operesheni hiyo ambayo inashirikisha mkoa wa Pwani na iliyo jirani walifanikiwa kuwakamata watuhumiwa hao pamoja na silaha mbili ambazo ziliporwa katika vituo vya Polisi vya Kimanzichana na Ikwiriri mkoani Pwani.

Alisema silaha ya kwanza ni SMG yenye namba TZPL 26686 ambayo iliporwa Juni 21, mwaka jana katika kituo cha Kimanzichana na nyingine yenye namba TZPL 26706 iliyotambuliwa kuporwa katika kituo cha Ikwiriri.

“Pamoja na silaha hizo pia zilipatikana risasi 23 za SMG na magazine mbili za bunduki hizo, katika kijiji cha Mandimkongo, wilaya ya Mkuranga,” alisema Kamishna Kova.

Akizungumzia kuhusu tukio la Ulatule, Kamishna Kova alisema, mtu huyo jana saa 4 asubuhi wakati akihojiwa katika Kituo Kikuu cha Polisi (Central) aliomba kwenda chooni na ndipo alipojirusha kutoka katika ghorofa ya tatu kwa lengo la kujiua au kutoroka.