Stori Kuhusu Mbwana Samatta Mara Baada ya Kutua Ubelgiji Kwenye Club ya Genk - MULO ENTERTAINER

Latest

29 Jan 2016

Stori Kuhusu Mbwana Samatta Mara Baada ya Kutua Ubelgiji Kwenye Club ya Genk

Mbwana Samatta, amewasili nchini Ubelgiji tayari kujiunga rasmi na Klabu ya KRC Genk inayoshiriki Ligi Kuu nchini humo.
Samatta aliondoka nchini juzi saa 6:00 usiku kuelekea Ubelgiji ili kukamilisha taratibu za kujiunga na klabu hiyo mpya ya Genk, baada ya bosi wa TP Mazembe, Moise Katumbi, kukubali kumuuza.
Meneja wa mshambuliaji huyo, Jamal Kisongo, alisema amewasiliana na Samatta na kumweleza kwamba amefika salama na ameanza kufuata taratibu zote ili aweze kufanya kazi nchini humo.
Alisema mara baada ya kuwasili, alitakiwa kufuatilia kibali cha kazi ambacho kitamruhusu kufanya kazi katika klabu hiyo mpya na muda wowote ataanza mazoezi.
“Kuhusu Hati ya Uhamisho wa Kimataifa) (ITC), Katumbi (Moise) amemhakikishia kuituma kwa klabu hiyo, kwani kabla ya kuondoka juzi aliongea naye na kumpa baraka zote za maisha mapya katika Klabu ya Genk,” alisema.
Kisongo alisema kwa kuwa bosi huyo wa TP Mazembe ameridhia kumuuza Samatta kwa Genk, siku chache zijazo anatarajia kwenda nchini Ubelgiji kwa ajili ya kusaini mkataba ambao atafaidika nao ikiwa mshambuliaji huyo atauzwa kwa klabu nyingine.
Samatta ambaye alitwaa tuzo ya kuwa Mchezaji Bora wa Afrika kwa wachezaji wa ndani, alikubali kujiunga na timu ya KRC Genk na kugomea ofa zilizotolewa na klabu za Nantes na Olympique Marseille za Ufaransa.