Safari ya Ulaya Imeiva – Ulimwengu - MULO ENTERTAINER

Latest

26 Oct 2016

Safari ya Ulaya Imeiva – Ulimwengu

Mshambuliaji wa Tanzania Thomas Ulimwengu aliyemaliza mkataba wake na klabu ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo amekiri tayari kuna vilabu kadhaa vya Ulaya ambavyo vimeonesha nia ya kutaka kumsajili.

Ulimwengu ambaye hakutaka kuongeza mkataba mwingine TP Mazembe amesema, anachosubiri kwa sasa ni wakati ufike ili aweze kusaini mkataba na kuanza maisha mapya barani Ulaya. Nyota huyo aliyecheza na Samatta kabla ya Samagoal kutimkia Ubelgiji hakuwa tayari kuvitaja vilabu vilivyoonesha nia ya kutaka saini yake, lakini akaahidi kila kitu kitakuwa wazi pindi atakapokamilisha usajili wake.

“Nilikuwa nimeshapanga tangu zamani kwamba, nikimaliza mkataba wangu na TP Mazmbe ni lazima nitoke kwasababu nilijaribu kutoka nikiwa ndani ya mkataba lakini ilishindikana kwahiyo nikapanga mkataba ukimalizika nitasogea mbele kwa ajili ya mafanikio zaidi, kilichobaki ni kuomba Mungu ili mambo yaende kama yalivyopangwa.”

“Ofa tayari zipo kilichobaki ni kukamilisha, ni kufikiria tu niende wapi na manager wangu kwa ajili ya kukamilisha mchakato.”

“Kwa sasa sifikirii tena kucheza Afrika, ila siwezi kuziweka wazi timu ambazo zinanihitaji, lakini baada ya kusaini kila kitu kitakuwa wazi.”

Faida aliyonayo Ulimwengu ni kuwa mchezaji huru kwahiyo sio lazima asubiri hadi dirisha la usajili lifunguliwe, kwa mujibu wa taratibu za FIFA, mchezaji ambaye amemaliza mkataba wake na timu aliyokuwa akiitumikia mwanzo, anaweza kusajiliwa kwenda klabu nyingine bila kusubiri kipindi cha usajili kufunguliwa.