UVCCM Wawajibu Vijana wa CHADEMA Kuhusu Tundu Lissu...Wawataka Waache Viherehere - MULO ENTERTAINER

Latest

10 Sept 2017

UVCCM Wawajibu Vijana wa CHADEMA Kuhusu Tundu Lissu...Wawataka Waache Viherehere

Umoja wa vijana wa Chama cha Mapinduzi CCM kupitia Kaimu Katibu Mkuu, Shaka Hamdu amewataka BAVICHA kuacha tabia ya kiherehere ya kuingilia taratibu za kitawala na kipelelezi pindi yanapotokea masuala mazito yanayohusisha moja kwa moja maisha ya watu

Kaimu Katibu Mkuu wa UVCCM, Shaka Hamdu akiwa pamoja na Kaimu Katibu wa Uhamasishaji wa Umoja wa Vijana UVCCM taifa.

Shaka amebainisha hayo leo ikiwa imepita siku moja tokea Mwenyekiti wa Baraza la Vijana Chadema (BAVICHA) Patrobas Katambi, alipotoa kauli yake ya kuwataka viongozi wote wa vijana wa chama hicho kushughulika na watu wanaoitwa 'wasiojulikana' ili waweze kutokomeza matukio ya kihalifu ambapo amedai pengine watu hao wananguvu kuliko vyombo vya dola na kuahidi endapo litashindikana jambo hilo basi atajiudhulu wadhfa aliokuwa nao katika chama chake.

"Umoja wa vijana wa Chama cha Mapinduzi CCM tunawakanya BAVICHA na kuwataka waache tabia ya viherehere ya kuingilia taratibu za kitawala na upelelezi pindi yanapotokea masuala mazito yanayohusisha maisha ya watu, kushambuliwa au kutekwa na wao wakataka kuyageuza kuwa ya kisiasa. BAVICHA wamejaribu kuyaunganisha matukio kadhaa walioyaita yamefanywa na watu wasiojulikana bila ya kufanya upelelezi wa aina yeyote na kutaja baadhi ya majina ya watu waliyokumbwa kwenye matukio hayo na kukwepa kutaja mfululizo wa mauaji ya viongozi wa CCM na serikali huko Kibiti mkoani Pwani", amesema Shaka.

Pamoja na hayo, Shaka amesema kwa mara ya kwanza UVCCM umemuunga mkono Mwenyekiti wa CHADEMA Mhe. Freeman Mbowe kwa kutoa matamshi ya kuwataka wananchi kutoonyesheana vidole juu ya tukio lililotokea huku akivitaka vyombo vya dola kuwajibika ipasavyo ili kubaini aliyetenda tukio hilo la kiuhalifu.

"Mbowe ametamka matamshi yaliyopevuka kifikra na kisiasa tofauti na povu lilivyo watoka vijana wake na kuonyesha uchanga katika siasa huku wakilitumia tukio la Lissu lenye huzuni kama jukwaa lao la kisisasa", amesisitiza Shaka.

Kwa upande mwingine, Shaka amewataka vijana wote Watanzania na wana CCM kumuombea dua Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu kwa yaliyomkuta ili aweze kupona na kurudi kuendelea na kushirikiana na Watanzania wenzake katika kulijenga taifa la Tanzania.