Serikali Yakataa Ombi la UKAWA Kutumia Uwanja wa Taifa kwa ajili ya Uzinduzi wa Kampeni Za Uchaguzi Mkuu - MULO ENTERTAINER

Latest

21 Aug 2015

Serikali Yakataa Ombi la UKAWA Kutumia Uwanja wa Taifa kwa ajili ya Uzinduzi wa Kampeni Za Uchaguzi Mkuu

SERIKALI imekanusha taarifa zilizojitokeza kwenye Vyombo vya habari yakiwemo magazeti na mitandao ya kijamii kwamba Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kitafanya mkutano hadhara Uwanja wa Taifa Dar es Salaam tarehe 22 Agosti, 2015.

Akizungumza na vyombo vya habari jana, Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Assah Mwambene alisema serikali haijatoa ruhusa kwa chama chochote cha siasa kutumia uwanja wa taifa kwa ajili ya shughuli za kisiasa

Alikiri kwamba ni kweli kwamba CHADEMA waliiandikia Wizara tarehe 12 Agosti, 2015 kutaka kutumia uwanja wa taifa katika uzinduzi wa kampeni lakini ombi lao lilikataliwa kwa maelezo kwamba uwanja ule kwa mazingira ya sasa hauruhusiwi kutumika kwa ajili ya mihadhara ya vyama vya siasa

“Kwa kipindi haturuhusu uwanja wa taifa kutumika kwa mihadhara ya kampeni za vyama vya siasa. Uamuzi huu unalenga kuweka uwanja katika mazingira rafiki ya michezo na kuepuka athari zozote zinazoweza kujitokeza kutokana na mihemuko ya kisiasa” alisema Bwana Mwambene.

Mwambene ameeleza kuwa, Serikali imeamua uwanja huo ubaki kwa ajili ya kufanyia shughuli zake za msingi za kimichezo ili kuepuka mihemuko na athari yoyote inayoweza kujitokeza kutokana na hamasa za kisiasa.

“Ni kweli kwamba tulipata barua ya Chadema kuomba Uwanja kutumika kwa ajili ya mhadhara ya kisiasa wa CHADEMA hasa kuzindua Kampeni zao kwenye Uwanja tayari tumeshawaandikia kuwaarifu kuwa Uwanja ule hauwezi kutumika kwa ajili ya shughuli zozote za kisiasa” alisema Bwana Mwambene.

Alisema vyama vyovyote vitakavyoomba kutumia Uwanja ule kwa shughuli za kisiasa havitaruhusiwa.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI