- MULO ENTERTAINER

Latest

8 Feb 2017

NAIBU Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson, `amemuumbua Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Dk. Hamis Kigwangalla baada ya kukanusha taarifa ya bohari za dawa kuwa haziko chini ya kiwango.
Naibu Spika huyo alilazimika kutoa maelekezo kwa serikali kuangalia Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG)juu ya ubovu wa bohari za dawa nchini na kuzifanyia kazi kasoro kama watazikuta.
Hatua hiyo ya Dk. Tulia ilitokana na Dk. Kigwangalla kukanusha taarifa ya bohari za dawa kuwa chini ya kiwango zilizotolewa na Mbunge wa Viti Maalum (CUF), Halima Ally Mohamed.
Mbunge huyo akiuliza swali la nyongeza, alisema kwa mujibu wa taarifa ya CAG ya mwaka 2014/15, kuna bohari zisizo na viwango na kutaka kujua msimamo wa serikali ili kuhakikisha afya za Watanzania.
Akijibu swali hilo, Dk. Kigwangalla alisema: “Kwanza, naomba nikanushe vikali sana kwamba kuna bohari za dawa zisizo na viwango. Hiyo ni ripoti ya CAG na hii ni taarifa ya serikali. Kwa hiyo naongea kama serikali kwa mamlaka kamili niliyopewa.”
Alisema bohari zilizopo ni za viwango vya hali ya juu na vimethibitishwa na Shirika la Kimataifa la Viwango (ISO), na zinakaguliwa kila baada ya miaka mitano na dawa haziwezi kutunzwa kwenye bohari zisizo na viwango kwa sababu zitaharibika.
“Dawa ni ‘high value items’ na hatuwezi kuzitunza ovyo, hivyo kwa sababu tunazitunza kwa gharama kubwa na ndiyo maana katika utunzaji, usambazaji mpaka katika kituo cha afya kijijini, kuna mnyororo uliokamilika unaozingatia viwango vya ubora,” alisema Dk. Kigwangalla.
Kufuatia majibu hayo, Dk. Tulia alisema: “Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa kuwa mbunge ameuliza taarifa zinazotokana na Ripoti ya CAG, serikali iangalie katika hiyo ripoti inasema nini ili kama alichosema mbunge kipo sawasawa ama hakipo sawasawa.”
Alisema kama kinachosemwa kipo kwenye ripoti, Wizara ya Afya iliangalie suala hilo.
Baada ya agizo hilo, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee, Watoto, Ummy Mwalimu, alisimama na kusema wamelipokea swali hilo na watalifanyia kazi.
Katika swali la msingi, Mbunge wa Mpwapwa (CCM), George Lubeleje, aliishauri serikali kuiwezesha Bohari ya Dawa nchini (MSD) kuwa na fungu maalum kutoka Hazina.
Akijibu swali hilo, Dk. Kigwangalla alisema MSD haiwezi kupewa fungu la moja kwa moja bila kupitia Wizara ya Afya.