Madam Wema Sepetu, Tusamehe tu Watanzania - MULO ENTERTAINER

Latest

17 Mar 2016

Madam Wema Sepetu, Tusamehe tu Watanzania

Naandika uzi huu kwa niaba ya Watanzania, kumhusu Madam Wema Sepetu, mlimbwende wa zamani wa Tanzania, akishinda Taji hilo mwaka 2006 mbele ya Jokate Mwegelo, mjasiriamali, msanii wa filamu, muziki na mwanaharakati na Lisa Jensen, aliyekuja kuwa Redds Miss World Tanzania mwaka 2012.

Kwa muda mrefu Madam amekuwa kwenye vichwa vya habari kwa wema na kwa ubaya, kama lilivyo jina lake, Wema Sepetu a.k.a Mama Ubaya, lakini ubaya ukionekana kuzidi wema wake machoni pa kundi la 'Watanzania Wastaarabu'.

Wema, kama washindi wengine wa taji hilo la Umiss, amelitendea haki kwa kufanya kazi zinazotakiwa, na walau kuka nalo vema hadi alipolikabidhi kwa mrithi wake, Richa Adhia mwaka 2007.

Wema Abraham Sepetu akiwa na Diamond Platinumz, msanii wa kimataifa wa Tanzania, enzi za mapenzi yao, kwenye Tuzo za MTV Afrika.​

Licha ya ushindi huo, madam amekuwa na 'kismati', kama wenyewe wanavyodai. Wachumba aliokuwa anatembea nao walipata mafanikio makubwa kwenye kazi zao, iwe muziki, uzalishaji au uigizaji wa filamu na pengine hata biashara zisizohusisha sanaa.

Ukikaa na Waridi utanukia, bila shaka mada amekuwa waridi kwa watu wengi, akiwaangazia nyota na kuwatangaza kimataifa. Madam akiwa upande wako, nani aliye juu yako? Kwa hili tuna deni kwake...

Madam amemsaidia sana msanii Diamond Platinumz, licha ya kuwa pumziko lake kwa miaka kadhaa, alimfundisha mambo mengi ya msingi ikiwemo lugha ya Kiingereza, nyenzo muhimu kwenye utandawazi.

Madam alimtoa Diamond kutoka uselebriti kunuka na kumfanya kuwa wa kisasa, msanii wa kimataifa. Popote tunapomsifia Chibu, tujue tuna deni kwa Madam Wema Sepetu.


Licha ya umaarufu wa magazeti na Blogu, madam ana juhudi binafsi za kimaisha, uzinduzi wa Kampuni ya Endeless Fame (inayomsimamia msanii Mirror), brand yake ya ' Kiss Lipstick' na maajabu mengine kibao.

Madam ni msanii, NDIO, mmoja wa wasanii wakubwa kabisa wa Bongo Movie... Tunapoona mafanikio yoyote kwenye tasnia, madam ana mchango wake mkubwa sana, kwa kweli anatudai.

Madam amewahi kushiriki kwenye Siasa ngazi ya kitaifa, kwa kugombea Ubunge Viti Maalum ndani ya Chama cha Mapinduzi. Licha ya kuwepo kwa dalili za ushindi wake kuchakachuliwa, alionesha uungwana wa hali ya juu kwa kukubali matokeo na kushiriki kikamilifu kwenye kampeni za Uchaguzi 2015.



Madam ni Celeb pekee kuwahi kuwa na Timu yake, timu inayojitambulisha kama #TeamMadam na ikijumuisha watu wakubwa na maarufu; Kajala, Petit Man, Aunt Ezekiel, DJ Rommie Jones (DJ wa Diamond Platinumz) na wengine wengi... Huu ni umaarufu wa Kiwango cha Kimataifa.


Licha ya kupumzika kidogo shughuli za filamu, bado hayuko nyuma kuwaunga mkono wasanii wenzake. Juzi alienda na gari lake kumpokea Elizabeth Michael Lulu, huu ni upendo uliopitiliza.

Madam ni mshiriki mzuri wa matukio ya kijamii na kindugu. Anahudhuria misiba, sherehe na matukio mengine kwa ukamilifu.Hata uhusiano wake na washabiki wake sio wa kunata wala kujidai, kama wadada wengine maarufu.

Sijasahau alivyojitolea kumtoa jela Kajala Masanja, wakati ambao wasanii wengine maarufu walipomsusa. Huu ni wema usio na kipimo...

Licha ya utu wake huu, madam amesakamwa na magazeti, blogu, mitandao na watanzania kwa ujumla. Wakimtusi, wakimkejeli, wakitengeneza picha za uongo, wakimuita malaya na wakati huo wakinufaika na kuuza habari zake.

Licha ya ubaya huu tuliomlipa, bado Wema ameendelea kuwa mzalendo, na mtu anayejitolea kwa taifa, kwa wasanii wenzake na jamii kwa ujumla. Kwa ambao wamewahi kuroll na Mama Lao, watakubaliana na mimi kuwa hayuko namna ambavyo watu wanamchukulia.

Kwa kweli wema wa Madam ungekuwa unaandikwa, vitabu vya dunia hii visingetosha kuuelezea wote.

Natoa wito kwa sisi kama taifa, kutafakari ubaya huu tuliomvika madame, na tumuombe radhi kwa ujumla wetu... Ikiwezekana tumjengee na mnara wa kumbukumbu.

By Mbilimbi Mbovu