Polisi Wafumua Kituo cha Wauza na Watumia Unga Jijini Dar es Salaam..Vijana 90 Mbaroni... - MULO ENTERTAINER

Latest

15 Mar 2016

Polisi Wafumua Kituo cha Wauza na Watumia Unga Jijini Dar es Salaam..Vijana 90 Mbaroni...

Jeshi la Polisi Mkoa wa Kipolisi Temeke, jijini Dar limekifumua kituo cha watumiaji wa madawa ya kulevya ‘unga’ na kuwakamata vijana zaidi ya 90 waliokutwa eneo hilo lililopo Mwembeyanga, Tandika.

Jumatano iliyopita mchana, polisi wakiwa na magari yao sita walivamia eneo hilo na kuwazunguka bila kutarajia kisha kuwashika na kuwapeleka Kituo cha Chang’ombe.

Gazeti hili lilishuhudia kamatakamata hiyo ambayo ilitokana na malalamiko ya wakazi wa eneo hilo ambao waliwatuhumu vijana hao kuwa licha ya kuvuta unga, lakini pia hufanya vitendo vingine vya kihalifu.

Zoezi hilo la kamatakamata linasemekana kuwa ni nguvu mpya ya kamanda mpya wa polisi wa mkoa huo ACP Gilles Muroto (pichani), ambaye amechukua nafasi ya ACP Andrew Satta aliyehamishiwa Kanda Maalum ya Polisi Tarime-Rorya.

Akizungumza na gazeti hili, Kamanda Muroto alisema msako huo mkali unaendelea katika mkoa mzima ikiwa ni pamoja na kuwasaka majambazi na akinadada wanaojiuza kwa jina maarufu machangudoa.